MAHUBIRI JUMAPILI YA KUPAA KWA BWANA MWAKA B


1.Mat1:1-11
2.Ef4:1-13
3.Mk16:15-20

TAFAKARI “ Yesu hamilikiwi na baadhi ya watu ila ni wa ulimwengu wote”
Jumapili ya leo tunaadhimisha sherehe ya kupaa kwa Bwana wetu Yesu Kristo mfufuka. Watu wengi wamekuwa na mawazo kwamba Kristu kupaa kwa Kristu kulikuwa ni kupotea mawinguni au hewani kwa sababu ya nguvu za kimungu alizofufuka nazo. Mawazo kama hayo huwa yanawapoteza wengi na hatimaye kuwafanya wasielewe mafundisho juu ya fumbo la kupaa kwa Bwana. Kristu kwa kupaa anamaanisha kuwa bado yupo na sisi kwa namna ya pekee.
Sikukuu ya kupaa kwa Kristo inamaanisha kuwa sasa Kristu hafungwi kwenye sehemu, kabila, au tabaka bali yeye sasa ni wa ulimwengu mzima. Kristu kupaa kwake anatufunulia kuwa anapatikana, katika viumbe vyote na duniani kote. Kupaa kwa Kristu Yesu hakumaanishi kuwa Kristu sasa hayupo nasi tena, bali ni kusheherekea Kristo kuwa pamoja nasi hadi ukamilifu wa dahali. Kristu yupo sasa katika jumuiya zetu, makazini mwetu, makanisani mwetu na kwa wale wote tunaokutana nao, hivyo ni jukumu letu kumfanya huyo Kristu aonekane pia kwa wale ambao bado hawajatambua uwepo wake katika maisha yao.
Mwinjili Marko katika injili yake hakuwa amejumuisha kipengele Mk 16:9-20 hivyo inaonekana kuwa ni kipengele kilichoongezewa baadaye katika hii injili kikiwa na maana yake na ujumbe mahususi kwetu sote. Kipengele hiki kilipata kuongezewa katika Injili ya Mtakatifu Marko ili kufanya fumbo la kupaa kwa Bwana lipewe umuhimu na nafasi zaidi katika imani ya waumini juu ya fumbo la ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristu. Wataalamu wa maandiko matakatifu waliweza kuongezea hicho kipengele ili kudhihirisha kuwa Kristu bado yupo kati yetu na kazi yake ya ukombozi inaendelea duniani kote.
Sherehe ya kupaa kwa Bwana inatukumbusha  wajibu wetu wa kuendelea kumhubiri na kumtangaza Kristu katika wale ambao hawajaonja upendo wake duniani kote. Kila mmoja wetu anaalikwa kuwa chombo cha utangazaji wa huyo Kristu aliyepaa kwa wote walio na kiu ya kumwona huyo Kristu katika maisha yetu ya kama wakristu wabatizwa.

Tunaalikwa kutambua kuwa Kristu yupo kwa viumbe vyote ulimwenguni tukianzia watu wanyonge katika jamii, kama vile maskini, wafungwa ( Mt25:34-46). Tutambue kuwa Kristu yupo kwa kila kiumbe hapa duniani. Mwaliko wa kutunza na kuhifadhi mazingira, raslimali za dunia ni mwito kwetu wakristu kupaza na kuinua sauti zetu dhidi ya wale wanaoharibu mazingira, japo hizo sauti kwa namna moja au nyingine huwa zinajaribu kuzimwa na watawala wenye uchu na kiu ya kupora hizo raslimali asilia. Sauti ya Kinabii inaenda mbele hata kwenye mifumo ya kisiasa isiyokidhi mahitaji ya binadamu, sauti ya kinabii inaenda pia zaidi kwenye mifumo ya kitabibu isiyo kidhi utu wa mwanadamu na baadala yake inaharibu utu wa mtu, mfano, utoaji mimba, kifo cha kujitakia, watoto wanazalishwa kwenye mifuko ( Test tube babies), Ni mazingira hayo tunamkuta Kristu. Sauti ya Kinabii ya Kanisa japo huwa mara nyingi inazimwa pia inajikita katika kutetea usawa juu ya mgawanyo wa madaraka na mifumo ya kiuchumi inayobagua walio nacho na wasio nacho katika mataifa mbalimbali ya dunia. Kristu ataendelea kuwepo katika maisha yetu pindi sisi kama wakristu tutakuwa katika nafasi ya kupaza sauti zetu katika mifumo ya Kijamii, Kisiasa, na Kiutamadauni ambazo kwa namna moja huwa zinakiuka maadili na utu wa mwanadamu. Hivyo ni mwaliko kwa kila mmoja wetu kutambua wajibu wake wa kumhubiri na kumtambua Kristu katika mifumo kandamizi isiyotambua utu wa mwanadamu katika jamii yetu tunayoishi.

Related Posts:

0 Response to "MAHUBIRI JUMAPILI YA KUPAA KWA BWANA MWAKA B"

Chapisha Maoni