MAHUBIRI YA KRISMASS

MAHUBIRI  YA  KRISMAS
MASOMO
I.Isa.52:7-10
II.Heb.1:1-6
III.Jn.1:1-18
TAFAKARI: UPENDO WA MUNGU KWETU UNAJIDHIHIRISHA WAKATI WA KUZALIWA KWA YESU KRISTU.
Tunavyotafakari kuzaliwa kwa mwokozi wetu Yesu Kristu, kadiri ya masomo jinsi yanavyotuongoza, tunapata picha kwamba Kristu anazaliwa katika mazingira ya kawaida tena mazingira hafifu, Katika kuzaliwa kwake Kristu anakosa hata nafasi katika nyumba ya wageni, na baadala yake anazaliwa katika holi la kulishia ngombe. Katika somo la kwanza, Isa52:7-10, tunasikia ujumbe na habari njema juu ya utabiri wa nabii ambapo nabii anasema kuzaliwa kwa Kristu kunaleta amani miongoni mwa wana wa Israel ambao walikuwa kwenye miangaiko na mifadhaiko. Amani iletwayo na Kristu ni ile amani ya ndani kwanza. Kuzaliwa kwa Kristu kwa wakati ule, kulibadili taswira, ya wakati ule ambapo chini ya utawala wa dola ya warumi, maovu , kama vile uzinzi, ndoa za jinsia moja, rushwa, ukosefu wa amani, upendo, mshikamano na haki  vilishamiri sana. Na Kristu kwa makusudi anazaliwa katika mazingira duni ambayo hata hayatamaniki kuzaliwa binadamu. Kristu katika kuzaliwa hivyo ilikuwa ishara kuonesha kwamba alizaliwa ili ashikamane na mazingira duni ya binadamu, ambapo pia kuzaliwa kwake katika mazingira duni ya namna hiyo ilikuwa ni pia kielelezo na taswira ya mazingira ya jamii ya utawala wa warumi ambao ulishamiri maovu mengi kama tulivyoona hapo kabla.
Mwanadamu katika kumtafuta Mungu hapo kale, tunaona kuwa wengine walimtafuta Mungu kila mahali, mfano jamii ya wamonaki hapo kale walijitenga na jamii na kwenda kuishi jangwani wakijaribu kumtafuta Mungu kuona kama angelipatikana  huko, wengine walimtafuta Mungu katika vituo vya hija n.k. Kwa leo tunapata ujumbe kuwa Mungu atafutwaye amekuja na yupo kati yetu, Yesu Kristu, yaani Immanuel, Mungu yu pamoja nasi yu katikati yetu. Ni maskini kama sisi ambapo wakati wa kuzaliwa kwake anazaliwa katika mazingira yasiyopendeza. Anakosa nafasi katika nyumba ya wageni. Kristu katika kuzaliwa kati yetu anakuwa mwanadamu kama wanadamu wengine, ili aweze kuishi ubinadamu huo na kuweza kujua mapungufu ya binadamu na hatimaye kukamilisha kile ambacho kinakosekana kwa mwanadamu, kwa maana hiyo ni kwamba ubinadamu wa Kristu unatusaidia kutuondolea ile dhambi ya Adam ambayo ilitufanya tuwe wana wa giza, na Kristu mwenyewe ambaye siyo mdhambi anatufanya tuwe wana wa nuru kupitia kushiriki ubinadamu wetu. Wale wote ambao humwamini huwa wana wa Mungu (Jn1:9-13)
Kristu, yaani Emmanuel kuzaliwa kwake kati yetu, ni ishara tosha ya maisha mapya na uhai, Kristu analeta uhai kati yetu, hasa kwa wale ambao wamekata tamaa, wamepoteza dira katika maisha. Tunaposheherekea kipindi hiki cha Krismas wengi wetu huwa tunanunua miti ya Krismas na pia kutengeneza mapango ambapo tunaona mwokozi anazaliwa humo. Mti wa Krismas kama tulivyosikia hapo awali, ni ishara ya uhai na maisha ya uzima usioharibika, na pango ambamo Kristu amezaliwa ni ishara ya kuzaliwa katika mazingira duni, na kwa jinsi hiyo Kristu anaungana nasi binadamu katika kushiriki na kutuinua kutoka katika mapungufu na madhaifu yetu.
Kristu kuzaliwa kwake anazaliwa kuwasha moto wa upendo kati yetu, anakamilisha kile ambacho kinakosekana kwetu sisi binadamu. Upendo umeshuka wakati huu kuwasha moto uwa upendo.  Katika kusheherekea kwetu sikukuu ya Noel, wengi wetu, tunajitahidi kutakiana amani, na upendo wa kuzaliwa kwa mwokozi  Yesu Kristu, tunadhihirisha hilo kwa kupeana zawadi na kupeana kadi za Krismas, hili hatulifanyi kutimiza wajibu wetu, ila linafanyika ili upendo ambao Kristu amekuja kuuwasha kati yetu uweze kudhihirishwa miongoni mwetu. Padri mmoja mjezuiti alipata kusema kuwa “ Baada ya mtu kupambana na misukosuko na kujua mwelekeo wa upepo, mawimbi na mivutano ya hapa na pale, Kama upendo wa Mungu umo ndani ya mwanadamu kiukamilifu, hivyo mwanadamu angeligundua moto kwa mara ya pili katika historia ya dunia” Wakati tunaendelea kusheherekea sikukuu ya Krismas pia basi ni mwaliko kwetu sote kuubeba upendo wa Kristu na kuupeleka majumbani mwetu, maofisini mwetu na katika maeneo yetu ya kazi.
Tusifikirie kuwa kuzaliwa kwa Kristu au kusheherekea sikukuu ya Krismas ni kula na kunywa tu, la hasha, wakati tunakula na kunywa pia tuwafikirie wale ambao hawana hata cha kuwasaidia katika maisha. Tunaalikwa kugawa huu mkate na kinywaji tunachokula wakati huu wa Krismas kwa wale ambao ni wahitaji. Sauti ya Mungu husikika kwa wale wamwombao kupitia kwa wale walionacho. Wakati huu tunaposheherekea Krismas basi kama mtoto Yesu anavyozaliwa katika mazingira duni,basi pia kwetu ni mwaliko pia kuwa karibu na watato ambao hawana haki zao za msingi kama vile malazi, elimu, na haki nyingine za msingi, watoto tuhakikishe kuwa wameandaliwa na wanasheherekea kumpokea mtoto Yesu katika mazingira ya upendo, furaha na amani.


Related Posts:

0 Response to "MAHUBIRI YA KRISMASS"

Chapisha Maoni